KAMWE USIKATE TAMAA MUNGU NDIYE HUPANGA MUDA WA WEWE KUPATA MTOTO

Share:
Image result for AFRICAN LOVER WITH BABY
Mada ya leo inajikita katika kuzungumzia manyanyaso, matusi na mambo mengi ya ajabu ambayo wanakutananayo wanandoa, hususan wanawake ambao wamekuwa wakibebeshwa mzigo mkubwa na mzito na wanaume wao.
Kinachonishangaza ni kuona binadamu anajivisha mamlaka ya kumtaka mwenza wake awe na mtoto ilihali anajua kabisa kuwa hilo hana mamlaka nalo isipokuwa Mwenyezi Mungu. Si ajabu pengine anayelalamika na kutukana kuwa anahitaji mtoto, yeye mwenyewe hana uhakika kama ni mzima kwa upande wa viungo vya uzazi au mwingine naye unakuta hata yeye hajajua kama akiolewa atapata mtoto au lah!
Mara nyingi chanzo cha tatizo hilo, lawama nyingi hubebeshwa upande mmoja wa wanawake, kwa kuamini kuwa mwanaume yeye huwa siku zote yuko sawa, hawezi kuwa na upungufu katika kukamilisha utungaji wa mimba.
Mbaya zaidi mwanaume anapojiona kuwa faragha yuko vizuri, ndiyo basi kabisa anaona hana sababu ya kushindwa kumlaumu mwanamke kuwa ndiye mwenye matatizo ya kutokushika mimba.
Moja kwa moja anaanza
 kulalamika na kumtuhumu mwenza wake kuwa yawezekana alitoa mimba nyingi kipindi cha usichana wake, mgumba au alitembea na mume wa mtu akafanyiwa figisufigisu.
Kumlaumu mwanamke kuwa ni chanzo cha mwanaume kukosa mtoto ni kumuonea. Kumlaumu mwenza wako kuwa ameshindwa kukuzalia mtoto bila wewe kufanyiwa uchunguzi wa kitabibu ni unyanyasaji wa kijinsia na ni kuingilia uumbaji wa Mungu. Hata kama akionekana ana tatizo, si vyema kumnyanyasa.
Zipo changamoto zinazowakumba wanandoa kwenye ndoa zao ikiwemo ugomvi wa mara kwa mara, malumbano ya hapa na pale na usaliti. Baadhi ya wanaume wamechukulia tatizo la kukosa mtoto kwa wenza wao kama fimbo ya kuwachapia wenza wao. Kila anapokosea jambo f’lani basi anaanza kusimangwa hata kama mwenye kosa ni mwanaume, lakini kibao kinamgeukia mwanamke.
Suala la mwanamke kutoshika mimba, pamoja na kwamba hata mwanaume anaweza akawa hana uwezo wa kuzalisha mbegu zenye uwezo wa kutengeneza mtoto, ni changamoto kwenye ndoa nyingi katika jamii.
Sehemu kubwa ya jamii inaamini kuwa wanandoa ambao wametimiza mwaka mmoja kwenye ndoa yao basi wanapaswa wawe na mtoto. Kama si mtoto, basi angalau mwanamke awe na mimba changa au kitumbo kiwe kimeanza kuonekana.
Ndugu yangu, si lazima kila ndoa iliyotimiza mwaka mmoja iwe na mtoto au mwanamke awe mjamzito. Suala la kupata mtoto ni uamuzi au majaliwa ya Mwenyezi Mungu. Wewe kama mwanamke huna mamlaka nalo. Wewe kama mwanaume, umebahatika kufunga ndoa na kuishi na mwenza wako, basi shukuru Mungu na hata suala la mtoto siku zote ni majaliwa ya Mungu na si upendavyo wewe.
Nayahisi maumivu makali anayopata mwanamke ambaye hana mtoto na mumewe badala ya kumfariji anageuka kuwa adui yake. Anageuka mtu wa kumnyanyasa. Inauma, inasikitisha na inatesa sana mioyo ya wanawake wengi.
Suala la mtoto limekuwa likizifanya ndoa nyingi kuingia kwenye mifarakano ya mara kwa mara kwa sababu tu haina mtoto au watoto. Mzazi wa mwanamke au mwanaume anahitaji mtoto, lakini katika uhalisia, pengine muda wa Mungu kuwazawadia zawadi hiyo kwenye ndoa yao haujafika.
Kinachoumiza ni kitendo cha baadhi ya wanaume na ndugu kuwabebesha lawama wanawake walioolewa na ndugu zao. Eti unakuta wifi anamsengenya mke wa kaka yake, mama mkwe naye anamnyali mke wa mtoto wake, ukiuliza, kisa unaambiwa “ndugu zake wanataka mtoto, yule mwanamke hana uzazi”. Kiukweli wanawake ambao hawajapata watoto huwa wanapitia mambo mengi kwenye uhusiano wao.
Kwa mwanaume mwenye upendo wa dhati kwa mwenza wake, hana sababu ya kumchukia mke kwa sababu hana mtoto au hajapata ujauzito. Kwanza anaanzaje kumuhukumu wakati yeye mwenyewe hana uhakika kama ni msafi kiasi cha kuhukumu?
Hata vitabu vitakatifu vinakataza kuhukumu kwani nawe utahukumiwa. Suala la kumlamu mwenza wako kutopata mtoto haliko kwenye uwezo wa kibinadamu.
Labda kama kuna sababu za kibinadamu ambazo pia inawezekana ni za bahati mbaya au kutokuelewa.
Naamini katika kumpenda na kumchagua kwako, ulikubali kuishi naye kwenye shida na raha, sasa inakuwaje kwenye tatizo hilo unataka kumuacha peke yake? Kwa nini unataka kumuongeza mwanamke mwingine kwa sababu uliyenaye hashiki mimba?
Hivi utajisikiaje kama mwenza wako siku moja akikukimbia kwa sababu tu umeishiwa ‘mpunga’? Bila shaka hutafurahia. Kama ndivyo, basi usimuhukumu kwa yeye kutokushika mimba badala yake mfarijiane katika kipindi hicho kigumu. Hata yeye mwenyewe anapenda kuwa na mtoto lakini hana uwezo wa kujitungisha mimba.
Wanawake wengine wanadiriki kuamua kuiba watoto hospitalini au kwenda kwa waganga ili wapewe dawa ya kupata watoto ili wawaridhishe waume zao, mawifi, mama au baba wakwe ambao wamekuwa wakiwatusi kuwa wanakula chakula cha bure cha ndugu yao na kujaza choo.
Maneno hayo yanauma, kumnyong’onyesha na kumuathiri kisaikolojia mwanamke.
Wanawake wanatukanwa matusi ya ajabu kwa sababu ya kukosa mtoto, wengine wanaingia mikononi mwa sheria na kufungwa kisa kikiwa kuiba mtoto. Uchungu wa mwanamke anayefungwa kwa ajili ya kukosa mtoto utakuwa wa maumivu makali.
Wanaume wengi mmekuwa mkiwalaumu wanawake kuwa ndiyo chanzo cha kushindwa kupata watoto wakati si kweli.
Kama mumeishi muda mrefu bila kupata mtoto nendeni hospitali mkapimwe huku mkimuomba Mungu

No comments